About KABENDE.COM

Manual Description Here: Ea eam labores imperdiet, apeirian democritum ei nam, doming neglegentur ad vis.

RIWAYA YA MWANAFUNZI MCHAWI SEHEMU YA 32 na 33

RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 32 na 33
Mtunzi:ENEA FAIDY
.... Shule ya sekondari Mabango ilikuwa na utulivu wa hali ya juu tangu Doreen alipoondoka shuleni pale. Licha ya kwamba kulikuwa na upungufu wa walimu lakini hali ilikuwa shwari kabisa. Wanafunzi waliendelea na masomo yao kama kawaida huku wakimshukuru Mungu kwa kuwaondolea mbaya wao aliyeisumbua shule ndani ya muda mfupi tu.
Majira ya saa saba mchana katika shule ile alifika Mwanaume mmoja wa makamo akiwa ameambatana na mwanamke mmoja mwembamba mrefu. Wanafunzi wa shule waliokuwa karibu waliweza kugundua kuwa mwanamke yule bila shaka alikuwa ni mama yake Dorice kwa jinsi walivyofanana. Nadia Joseph aliyekuwa anapita eneo lile la ofisi aliwasalimia kwa heshima kisha akasimama kidogo huku akitafakari jambo alilotaka kuzungumza.
"Samahani mama.. We ni ndugu yake Dorice.." Aliuliza Nadia huku akitabasamu.
"Ndio.. Ni mama yake mzazi.." Alijibu mama yule.
"Oh mmefanana sana... Vipi lakini hajambo?" Aliuliza Nadia akiwa anatabasamu lakini swali lile lilikuwa kama mwiba mkali moyoni mwa Mama Dorice kwani ujio wake pale shuleni ilikuwa ni kumfuata Dorice na kupata taarifa zake kwani ulipita muda mrefu sana bila mawasiliano yoyote.
"Kwani Dorice hayupo hapa shule?" Aliuliza Mwanaume aliyeambatana na Mama Dorice kwa mshangao. Na huyo alikuwa ni mjomba wa Dorice.
"Ah! Unataka kuniambia hayupo nyumbani?" Alishangaa Nadia lakini ndani ya muda mfupi alitokea madam Amina eneo lile hivyo Nadia aliamua kuondoka ili kukwepa adhabu.
Madam Amina aliwasogelea wageni wale na kuwasalimu. Kisha akawakaribisha ofisini. Bila kuchelewa wageni wale waliambatana na Mwalimu Na kuingia ofisini.
"Karibuni sana.. "
"Asante.. Sisi ni wazazi wa Dorice na tumekuja hapa kuuliza binti yetu anaendeleaje?"
"Dorice.. Alikuwa kidato cha nne?" Aliuliza mwalimu.
"Ndio!"
"Mmh! Mbona aliacha shule na tuliwapigia simu mkasema amefika" alisema Mwalimu Amina kwa mshangao. Kauli ile iliularua moyo wa mama Dorice na kumfanya achanganyikiwe sana, maana hakuna simu aliyopigiwa wala Kuambiwa chochote kuhusu mwanae.
"We mwalimu umechanganyikiwa? Mbona kama hujielewi eti?" Mama yule wa kinyaturu aliinuka kitini na kuanza kumfokea mwalimu.
Mwalim Amina aliamua kujitetea kwani hali ya hewa ilianza kuchafuka ofisini mle. "Tunamtaka mwanetu.. Mmemtorosha nyie? Au mmemuua?" Alizidi kucharuka mama Dorice.
Mwalimu Amina alikumbuka mbali, akakumbuka siku ambayo Dorice alipotea kisha wakapewa taarifa za upotevu wa mwanafunzi huyo. Barua ya maelezo iliandikwa kisha walimu wakapiga simu kwa wazazi wa Dorice. Lakini kwa bahati mbaya sana simu ilipokelewa na jini Mansoor kwa namna ya ajabu sana. Na jini huyo aliongea sauti ya Mama Dorice na kuwafanya walimu wajiaminishe vizuri kuwa waliongea na mama Dorice lakini kumbe haikuwa hivyo na hakuna aliyejua siri hiyo zaidi ya Mansoor pekee.
"Mama tena nilipiga simu Mimi.. Na ulikubali mwanao aache shule.." Alijitetea madam Amina lakini hakueleweka.
Wazazi wa Dorice waliondoka kwa hasira sana shuleni pale huku wakiwa hawajui binti yao alienda wapi. Roho iliwauma sana lakini hawakuwa na jinsi. Waliondoka na gari yao waliokuwa wamekodi ikawafikisha kituo cha mabasi Iringa mjini.
Walishuka ili watafute sehemu ya kula chakula kwani hawakula chochote tangu asubuhi kisha wakate tiketi, ghafla kwa mbali sana Mama Dorice alimwona msichana kama Dorice. Alijifuta macho yake na kutazama vizuri akamtazama vizuri binti yule.
"Kaka Dorice yule pale"
"Yuko wapi?" Kaka yake alishtuka sana.
"Pale mbele kwenye watu wengi.. Tumfate haraka.." Alisema Mama Dorice akiwa tayari ameanza kupiga hatua kuelekea kule alipo msichana yule.
********
"Chukua hii" Bi Tatile alimpa hirizi moja Doreen. Doreen aliipokea kwa mkono wake wa kushoto na kusikiliza maelekezo kwa umakini kutoka kwa Bi Tatile.
"Hii umeze sasa hivi.... Haraka sana.." Aliamrisha Bi Tatile na Doreen alifanya hivyo haraka. Akaibugia mdomoni na kuimeza. Alihisi maumivu makali sana ya Tumbo, akapiga kelele kwa kulalama.
"Hapa inabidi urudi haraka nyumbani... Ukajisaidie haja kubwa sebuleni kwenye sahani safi.. Kisha uzunguke sebuleni Mara Saba kutokea kona moja hadi nyingine huku akitamka jina la msichana yule... Umenielewa?"
"Nimekuelewa mtukufu.." Alijibu Doreen kwa woga kiasi.
"Haya ondoka haraka.." Aliamrisha Bi Tatile huku akimalizia na kicheko kikali cha kutisha.
Bila kuchelewa Doreen aliopotea eneo lile na kutokea nyumbani kwa Mama Pamela. Pindi alipokuwa anaingia ndani kilisikika kishindo kizito sana. Doreen aliingia ndani na kupulizia dawa ya kuwalaza usingizi wote waliokuwa ndani kisha akaenda sebuleni. Akachukua sahani nzuri sana Kabatini, akaiweka chini na kujisadia haja kubwa yenye harufu Kali sana kwenye sahani ile. Kisha akaenda kwenye kona ya kwanza na kuanza mzunguko wa kwanza huku akitamka jina la Pamela.
Akamaliza mizunguko saba kama alivyoambiwa punde Pamela alitokea sebuleni pale. Doreen alicheka kicheko kikali sana cha kutisha, huku akimsogelea Pamela aliyekuwa ameinamisha kichwa chino bila kumtamzama Doreen.
Doreen alisigeza mkono wake na kuusogeza kifuani kwa Doreen kwenye titi lake la kushoto. Akalishika titi lile huku akitamka maneno Fulani kisha titi lile likapotea kifuani kwa Pamela akabakiwa na titi moja tu. Pamela alikuwa hajielewi kabisa akiwa pale. Baada ya titi kuchukuliwa akapotea. Na Doreen pia akapotea huku moyoni mwake akifurahia ushindi alioupata kwani tayari kazi iliyomleta ilikuwa imekamilika.
Asubuhi na Mapema, Mama Pamela aliamka usingizini akiwa mchovu sana. Alijikongoja na kwenda chumbani kwa mwanaye alikuta amelala fofofo, akamshtua.
"Mbona umelala sana Leo?"
"Mama naumwa sana." Alisema Pamela kwa sauti ya kichovu.
"Unaumwa? Unaumwa nini? " mama Pamela alishangaa.
"Kifua kinaniuma sana.. Titi linauma balaa.."
"Titi?" Alishtuka mama Pamela.
"Ndio.."
"Pole sana.. Halafu kuna harufu naisikia humu ndani.. Sijui pua zangu.." Alisema mama Pamela na kulipuuza suala la binti yake kwani alihisi ni ugonjwa wa kawaida tu.
"Hata Mimi naisikia..." Alisema Pamela.
"Ngoja niangalie angalie basi huko sebuleni." Alisema Mama Pamela na kwenda sebuleni. Alipoingia tu alikaribishwa na harufu mbaya sana iliyomfanya apige chafya. Na kwa ukali wa harufu ile alitamani atapike. Macho yalitua moja kwa moja mpaka kwenye sahani yake iliyokuwa imejaa kinyesi pale sebuleni kwake.
"Oh My God!" Alishtuka Mama Pamela huku macho yamemtoka kama yai la kisasa.
"Ama kweli dunia ina mambo.. Pamelaaa! Njoo!" Alisikika mama Pamela.
Pamela aliitika na ndani ya sekunde chache alifika sebuleni pale.
"Oh gash! Nani kafanya ivi?" Alishangaa Pamela baada ya kushuhudia tukio lile pale sebuleni.
"Shangaa wewe! Maana mie nimeishiwa nguvu kabisa!" Alisema mama Pamela. Walishangaa kupita kiasi na muda si muda Doreen alifika sebuleni sebuleni pale na kuungana na wenye nyumba kushangaa tukio zima.
"Alaaniwe sana aliyefanya tukio hili.." Alisema Doreen huku akipiga makofi ya mshangao.
"Halafu Dada Pamela hapo kifuani pakoje?" Aliuliza Doreen.
Pamela alishtuka kusikia swali lile. Akajiangalia kifuani kwake na kugundua kifua chake kimetuna upande mmoja lakini upande mwingine hauna kitu. Hofu kuu na mshangao vikamvamia akajifunua shati na kujikagua zaidi.
*********
"Mama Eddy.. Nashukuru sana mdogo wangu kwa ulichonifanyia... Mungu tu ndo anaejua.... Kwaheri." Alisema Dada yake mama Eddy na kutoka sebuleni Pale.
Mr Aloyce alijtahidi kumzuia asiondoke ilishindikana. Mwanamke yule aliondoka kistaarabu na kuwaachia nyumba yao.
"Mke wangu ulichofanya sio ustaarabu.." Alisema Mr Alloyce.
"Ustaarabu haulipwi... Kwahiyo hauna faida.." Alijibu mama Eddy na kukaa kitini.
"Mh! Sawa..."
"Hebu tuachane na yaliyopita kuna jambo nataka nikuambie.
"Mama kwanini umefanya vile? Mbona umebadilika sana?"
"Na wewe sitaki kelele... Hebu ondoka hapa niongee na mume wangu.."
"Sawa lakini mamkubwa alikuwa tatari kunisaidia tatizo langu" alisema Eddy.
"Ulimwambia sio?"
"Ndio..." Alijibu Eddy kwa hasira na kutoka sebuleni pale akiwaacha na mazungumzo yao. Roho ilimuuma sana Eddy kwa kitendo alichofanya mama yake, lakini hakuwa na jinsi.
"Nisikilize mume wangu mpenzi.." Alisema ma Eddy.
"Sema"
"Nataka tumrudishe Eddy shuleni... Maana masomo yanampita sana.."
"Unasemaje? Vipi kuhusu tatizo lake?"
"Hilo lishakuwa la maisha cha msingi arudi shule"
"Hapo sijakuelewa mke wangu.. Si ni bora tumpeleke hata kwenye maombi?" Alisema Baba Eddy na katika vitu alivyovichukia mama Eddy yule wa bandia ni suala la maombi.
"Maombi kitu gani? Unawaamini wachungaji wenyewe waongo tu? Sitaki maombi kwa mwanangu asije akatupiwa majini bure..." Alisema mama Eddy.
"Kuombewa ataombewa tu... Tena nimekumbuka kitu..." Alisema Mr Aloyce na kunyanyuka kitini pale haraka..
SEHEMU YA 33
...BAADA ya kujikagua kwa muda Pamela aligundua hana titi lake moja la kushoto. Jasho jembamba lilimtiririka kwa kasi ya ajabu. Hakutaka kuamini kile alichokiona, akaanguka chini ghafla na kupoteza fahamu. Mama Pamela alipigwa na butwaa la ajabu, uvumilivu ukamshinda akamwita Pamela Mara kadhaa lakini Pamela hakuitikia. Kwa mshtuko alioupata pia mama Pamela alidondoka chini Puuh! Kama mzigo na kupoteza fahamu palepale.
Doreen alisimama pembeni yao, alicheka kwa kiburi sana kisha akaondoka zake sebuleni na kuingia chumbani kwa mama Pamela moja kwa moja. Aliingia chumbani kinyumenyume kisha akatamka maneno Fulani halafu akageuka na kusogelea kitanda cha Mama Pamela, akatazama chumba kizima kisha akagundua sehemu yenye pesa. Akatikisa kichwa na kuisogelea droo moja ya 'dressing table' na kuchukua pesa zote zilizokuwemo mle. Na droo ile ndio ambayo aliitumia mama Pamela kuhiffadhi pesa zote.
Bila huruma Doreen alichukua pesa zote alizozikuta mle, zilikuwa takribani laki tano kisha akaenda chumbani kwake na kubadili nguo haraka kisha kisha akachukua begi lake dogo akaondoka zake.
Doreen alitembea mwendo wa haraka sana mpaka alipofika barabarani na kupanda daladala inayoelekea stendi kuu ya Nanenane.
Mama Pamela na mwanaye walilala pale chini kwa muda wakiwa hawajitambui. Ndani ya nusu saa nzima ndipo mama Pamela alipopata fahamu na kuwezs kuinuka, alikaa dakika tano nzima ndipo kumbukumbu zikamrejelea. Machozi yalimdondoka huku akiinuka na kwenda kuchukua simu kitu cha kumpepea mwanae ili azinduke. Alichukua khanga laini na kuanza kumpepea Pamela mpaka alipozinduka. Lakini muda wote huo kuna kitu alikifikiria na alihisi kimepungua mle ndani. Akawaza kwa muda ni kitu gani hicho ndipo akakumbuka kuwa hakumwona Doreen.
"Doreen! Doreen!" Aliita mama Pamela lakini hakusikia sauti yoyote iliyoitikia. Akaachana nae akijua labda yupo nje.
"Mama siamini! Sitaki kuamini kilichonitokea!" Alisema Pamela huku akilia.
"Sijui nani amefanya hivi?" Aliuliza mama Pamela.
"Mama! Kuna ndoto niliota... Ila sikudhani kama ni kweli kumbe ilibeba ukweli mzito sana!" Alisema Pamela kwa huzuni huku akilia.
"Ndoto gani hiyo? Na je ulimwona Mtu yeyote?"
"Ndio mama nilimwona!"
"Alikuwa nani?"
Kabla Pamela hajasimulia chochote kuhusu ndoto aliyoota, simu ya Mama Pamela iliita na kumfanya ainuke haraka na kwenda kuifata simu yake. Mpigaji alikuwa ni Baba Pamela, mama Pamela alipokea simu huku huzuni ikimzidia.
"Haloo mume wangu..."
"Halloo... Habari za huko?"
"Mmh.. Za huku si nzuri...!"
"Mh! Kwanini?" Alishtuka baba Pamela. Mama Pamela akamsimulia kila kitu kilichotokea nyumbani kwake tangu alipoondoka. Mkasa ule mzito ulimshangaza sana Baba Pamela, alikuwa haamini kabisa kilichomtokea binti yake.
"Ina maana Pamela hana titi moja sasa?"
"Ndi..ndioo..."
"Unaona sasa mke wangu? Nilikwambiaje Mimi?? Nilikwambia nini kuhusu yule mgeni wako?" Baba Pamela alianza kumlaumu mkewe kwa kutokuwa mwelewa lakini suala lile likazua ubishi kwa mama Pamela kwani hakuamini kabisa suala la Doreen kuhusika ns ushirikina.
"Mume wangu... Unamkosea Mungu kumhusisha yule binti na ushirikina, yule mtoto ni mpole tena mstaarabu.." Alisema mama Pamela.
"Tatizo lako mke wangu ni hilo... Hutaki kuukubali ukweli na ndio maana umesababisha matatizo kwa mwanangu bora yangekukuta we we.." Alisema Baba Pamela.
"Baba Pamela mbona we king'ang'anizi hivyo? Doreen sio mchawi... Waliofanya hivyo watakuwa ni majirani tu..."
"Mh umenishinda we mwanamke." Baba Pamela alikata simu kwa hasira.
Akili ya Mama; amela ilikuwa ngumu sana kuamini maneno ya mumewe. Alijua mumewe anamsingizia tu binti wa watu, mtoto mwenye adabu kupita kiasi, mchapakazi tena mwenye hekima. Hivyo ndivyo mama Pamela alivyomchukulia Doreen bila kujua upande wa pili Doreen alikuwa ni mtu wa aina gani.
"Hebu nisimulie vizuri hiyo ndoto yako Pamela.."
"Mama tuondoe kwanza hicho kinyesi maana harufu yake inanisumbua sana..." Alisema Pamela.
Mama Pamela alienda jikoni na kutafuta mifuko ya plastiki kisha akajivalisha mikononi halafu akaenda kubeba ile sahani yenye uchafu kutoka tumboni mwa MTU mwingine na kuubeba kwa kinyaa sana kisha akaenda nao nje. Alitafuta eneo zuri na kuchimba shimo dogo akafukia uchafu ule pamoja na sahani. Alinawa mikono kisha akarudi tena sebuleni ambapo bado palikuwa na harufu Kali. Akawasha kiyoyozi na kufungua madirisha yote kisha harufu ile ikaanza kuaga Nyumba taratibu sana na kwa maringo yaliyokithiri.
Baada ya kuhakikisha usalama wa nyumba yake mama Pamela akaketi kitini na kumsikiliza mwanaye.
****
Baba Eddy alisogelea droo yake ya kuhifadhia vitu na kuchukua kijidaftari kimoja kidogo amabacho Mara nyingi alikitumia kuhifadhia namba za simu za watu wake muhimu. Baada kukipata alienda nacho sebuleni na kuketi kitini huku akikipekuapekua kwa uangalifu.
"Nimefanya uzembe kwa muda mrefu lakini sasa nimegundua njia sahihi ya kumtibu mwanangu..." Alisema Mr Aloyce.
"Kwani njia gani umeigundua? Kuna daktari unamfahamu?" Aliuliza mama Eddy.
"Kwahili suala halihitaji daktari..."
"Mh kivipi... Basi mganga...!"
"Mganga wa nini? Umesahau kilikutokea tulipotaka kwenda kwa mganga?" Alisema Baba Eddy huku akizinakiri namba Fulani kutoka kwenye kile kijidaftari na kuweka kwenye simu yake.
"Mbali na hao... Unafikiri nani atatusaidia mume wangu? Hakuna mwingine... Tusipoenda kwa daktari basi ni kwa mganga tu.." Alisema mama Eddy kwa sauti ya ushawishi sana lakini haikumwingia akilini hata kidogo baba Eddy.
"Hao uliowasema watashindwa... Cha msingi ni kumtegemea Mungu tu..."
"Unampigia Mchungaji?" Alishtuka mama Eddy.
"Ndio.." Aliitikia Baba Eddy na tayari muda huo huo alipiga simu na ikaanza kuita.
"Wewe mbona upo ivo? Mchungaji wa nini sasa? Hatokusaidia kitu zaidi ya kupoteza muda.. Hebu kata simu.." Alisema mama Eddy huku akimnyang'anya simu mumewe na kukata. Baba Eddy alimshangaa sana mkewe. Alijikuta anamtandika Kofi zito sana la usoni bila kutarajia.
"We mwanamke ni mchawi nini? Kwanini ukatae maombi ya watu wa Mungu?" .
Mwanamke yule alipiga ukunga kwa maumivu. Akajishika shavu lake kwa kuugulia kipigo kile.
"Unanipiga Mimi?" Alisema mama Eddy. Mr Aloyce alibaki kimya tu bila kusema neno kwani alikuwa na hasira sana. Alichukua simu yake na kuondoka sebuleni pale, akaingia chumbani. Haukupita muda kabla hata hajapiga simu tena mama Eddy aliingia chumbani.
"Si umenipiga? Sawa! Wewe ni mbabe! Ila nitakuonesha!" Alisema Mama Eddy na kuzidi kumtia hasira zaidi Mr Aloyce.
"Sitaki masikhara kwenye vitu vya msingi ondoka huku chumbani!" Alisema Mr Aloyyce huku akijaribu kupiga tena simu.
"Mume wangu... Nisamehe basi... Tuyamalize basi baby!" Alisema mwanamke yule kwa sauti ya mahaba utadhani sio yule aliyekuwa na hasira hapo mwanzo. Alimsogelea mumewe kimahaba na kumyang'anya simu mumewe kisha akamteremshia mvua ya mabusu mdomoni mwake.
"Nakupenda mume wangu..." Alisema mwanamke yule akiwa amekata simu na kuiweka pembeni. Mr Aloyce alibaki kimya akimtazama tu mkewe kwa mambo anayoyafanya. Mwanamke yule aliendelea kumpapasa mumewe akiwa na lengo la kumfanya Mr Aloyce apoteze wazo la kumpigia simu mchungaji. Kwani alifahamu vizuri nguvu ya maombi ya watu wa Mungu na jinsi ambavyo angeshindwa kufanya kazi yake.
Licha ya kutumia mtego ule kwa Mr Aloyce lakini bado ilishindikana kumfunga akili yake ya kumpigia simu mchungaji. Mr Aloyce alisukuma kwa nguv na kuchukua simu yake kisha akaenda chumba cha wageni na kujifungia mlango, akampigia simu mchungaji. Alipopokea tu simu ile, ghafla mlango wa chumba ukafunguliwa. Mr Aloyce alishtuka sana, kwani alikuwa amefunga mlango na funguo. Mkewe aliingia.
"Mchungaji.. Naitwa Mr Aloyce... Nina matatizo makubwa sana kwenye familia yangu nahitaji maombi mchungaji tafadhali..."
Alijieleza mr Aloyce kabla hata ya salamu. Lakini muda huo alisikia sonyo Kali sana kutoka kwa mkewe, na hakuelewa ni kwanini mkewe alisonya kidharau kiasi kile kisha akatoka chumbani mle.
*****
Mama Dorice alitembea mwendo wa haraka sana na kumkaribia msichana yule aliyedhani kuwa ni mwanaye. Alimkaribia msichana yule na kumwita "Dorice!" Msichana yule akageuka na kumtazama aliyemwita ndipo mama Dorice aliposhtika sana baada ya kugundua binti yule hakuwa Dorice.
"Samahani binti nimekufananisha.." Alisema mama Dorice na kumgeukia kaka yake ambaye alikuwa anamfata kama Bendera inayofuata upepo.
"Dada mbona sikuelewi..?" Aliuliza mjomba wake Dorice.
"Kaka acha tu...."
"Kwani vipi?"
"Nilimwona Dorice kabisa lakini nilipofika hapa kumbe sio...."
"Umemfananisha?"
"Nadhani..."
"Haya twende basi tukate tiketi... Turudi nyumbani tuangalie ni jinsi gani ya kumpata mwanetu.... Maana hatuwezi sema alifariki bila uchunguzi labda aliacha shule akaolewa?"
"Ila sidhani kama inawezekana Dorice aolewe kizembe ivo... "
"Usikatae dada yote Yanawezekana..." Alisema mjomba.
Waliondoka eneo lile na kwenda moja kwa moja kwenye mgahawa mmoja ambapo walipata chakula kisha wakaenda kukata tiketi ya basi. Walipokuwa pale , mama Dorice alimwona tena MTU kama Dorice akiwa amevaa mavazi Yale yale kama ya yule aliyemwona mwanzo.
Mama Dorice alishtuka. Akamtazama kwa makini binti yule akagungua ni yeye kabisa tena cha ajabu binti yule alimpungia mkono huku akitabasamu. Na alikuwa amependeza kupita kiasi gauni refu jekundu alilovaa, pamoja na viatu virefu vya bluu alivyovaa vilivyoenda sambamba na mkufu na hereni zake. Huku nywele zake ndefu zilizojimwaga zikimfanya aonekane maridadi zaidi.
Mama Dorice hakulaza damu akaamua kumfuata haraka binti yule lakini cha ajabu
ITAENDELEA.....
Read More...

RIWAYA YA MWANAFUNZI MCHAWI SEHEMU 31

RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 31
Mtunzi:ENEA FAIDY
...Doreen alimsikiliza kwa Umakini mama Pamela ili ajue ni swali gani analotaka kuuliza. Mama Pamela alikaa vyema kisha akakohoa kidogo na kumtazama Kwa makini Doreen.
"Niulize Tu mama" alisema Doreen.
"Hivi ni kitu gani unapenda nikufanyie ili moyo wako ufurahi? Maana nimependa sana heshima na adabu uliyojaaliwa." Alisema mama Pamela.
"Kiukweli mama Mimi napenda sana unitafutie shule.. Ili niweze kusoma na kufikia malengo yangu" alisema Doreen.
"Shule tu? Wala usijali wiki ijayo nitakuwa tayari nimetafuta shule kwa ajili yako.."
"Nitafurahi sana mama..."
"Unapenda shule ya kutwa au bweni?"
"Yoyote tu itanifaa" alisema Doreen.
Suala lile lilimfurahisha sana Doreen, aliendelea kuishi kwa kunyenyekea sana ndani ya nyumba ile, lakini katika ulimwengu mwingine alikuwa ni mtu jeuri na katili kwa familia ile. Kila Mara aliliwinda sana titi la Pamela, alitamani kulipata kwa udi na uvumba lakini kwa bahati mbaya ilikuwa vigumu kulipata. Alitumia kila namna lakini bado hakuelewa sababu ya kushindwa kulipata titi la Pamela.
Hasira zilimuwaka sana Doreen pale alipoingia chumbani kwa Pamela usiku na kutaka kumkata titi lake. Alikuta Pamela amelala usingizi mzito sana, akampulizia dawa ili usingizi ule uzidi kuwa mzito zaidi kisha akamsogelea taratibu akiwa ameshikilia panga Kali lililofungwa kaniki nyeusi na nyekundu.
Doreen alitamka maneno ambayo aliyajua mwenyewe kisha akamfunua shuka Pamela na kusogeza kisu chake karibu na titi la Pamela. Hakuwa na hofu kama kazi yake haitofanikiwa kwani alikuwa anajiamini na alikiamini kile alichokifanya. Lakini kwa bahati mbaya sana kila alipotaka kumgusa Pamela na upanga ule, Doreen hakuona chochote kitandani pale. Alijaribu tena na tena lakini bado hali ikaendelea kuwa vile vile. Doreen alikasirika sana, akatupa chini upanga ule mlio wake ukamshtua Pamela usingizini.
Doreen alishtuka sana baada ya Pamela kushtuka usingizini, akakimbia haraka na kujibanza kwenye kona moja ya chumba kile kisha akatamka maneno Fulani ya kichawi halafu akatulia kimya.
Pamela aliangaza macho huku na kule chumbani mle lakini hakuona kitu, akainuka kitandani na kuwasha taa kisha akaangalia kila sehemu ya chumba kile lakini hakuona chochote. Akatoka na kwenda msalani, alipokuwa anajisaidia haja ndogo akahisi kuna mtu anamfuata nyuma yake Pamela alishtuka na kuogopa sana kisha akakumbuka jambo muhimu la kufanya kama alivyoambiwa na baba yake. Pamela akasali kwa sauti ya chini na kwa imani kubwa sana kisha akajisaidia na kurudi kitandani, akalala bila kuzima taa.
Doreen alikasirika sana baada ya kumkosa Pamela kwa Mara nyingine. Akaamua kurudi chumbani kwake kupitia kona ile ile aliyokuwa amejibanza.
Doreen alitokea chumbani kwake akiwa na hasira sana. Alijituliza kimya akiwa amekaa chini sakafuni huku akiwa ameshika tunguli na hirizi mkononi mwake. Aliamua kuita mizimu ya kwao ili iweze kumsaidia katika hali ngumu aliyonayo.
Ndani ya sekunde chache alitokea mwanamke mmoja Mzee sana. Kichwa chake kilikuwa kimejaa mvi lakini hakuvaa nguo yoyote isipokuwa kaniki nyeusi aliyovaa kiunoni pamoja na shanga nyingi sana alizokuwa amevaa kiunoni mwake na shingoni. USO wake ulikuwa na makunyanzi mengi sana yaliyokuwa yametawaliwa na vitu kama unga unga mweupe. Alipotua tu chumbani kwa Doreen, nyumba nzima ilitikisika kwani alikuwa ni mtu mkubwa sana katika himaya ya uchawi ya akina Doreen.
"Karibu! Karibu! Mama mtukufu! Mkuu wa wachawi wote! Mwenye nguvu kuliko wote duniani!" Doreen alimkaribisha mgeni wake yule kwa heshima kubwa sana. Yule bibi hakutoa sauti yoyote zaidi ya Kuitikia kwa kichwa tu huku akimsogelea Doreen kwa kutumia makalio yake.
"Doreen! Tangu tumekutuma huku duniani hujawahi kuniita isipokuwa Leo.. Najua una jambo zito linalokusumbua"
"Ndio! Ndio! Mtukufu"
"Sasa inabidi tutoke humu maana si mahali sahihi"
"Sina pingamizi Bi Tatile! Kipenzi cha wachawi wote" yule Bibi alimshika mkono Doreen kisha taratibu kwa kutumia makalio yao wakasogelea kona ya kushoto kwao. Kisha wakatoweka ndani ya jumba lile. Lakini kitandani kwa Doreen waliacha mwili wa Doreen pekee na hata kama angeamshwa kwa kipindi kile basi asingeweza kuamka .
Safari ya wawili wale kwa kutumia usafiri wa ungo huku dereva akiwa Bi Tatile iliwafikisha mpaka eneo la makaburini ambapo walitua na wakaketi hapo kisha wakaendelea na kikao chao kifupi kilichotokea kwa dharula.
"Sema mjukuu wangu.. Mimi ndo Tatile binti Matatila mwenye uwezo wa kubadili nyasi za kijani zikawa nyeupe.."
"Mtukufu lile suala la kupata titi naona linakuwa gumu sana kwangu.. Nimekamilisha kila kitu lakini bado hilo tu.. Tafadhali naomba unisaidie kwa hili..."
"Ha ha ha hah Doreen wewe una uwezo mkubwa sana wa kukamilisha hilo.. Unaweza ukafanya hivyo haraka sana ila kuna jambo moja tu! Unatakiwa ufanye."
"Jambo gani mtukufu? Niambie tu maana nimechoka kuhangaika" alisema Doreen. ****
Majira ya saa kumi na moja jioni Dada wa Mama Eddy aliwasili nyumbani kwa Mr Aloyce. Alipokelewa vizuri sana na Bwana Aloyce pamoja na Eddy lakini ilikuwa tofauti sana kwa mama Eddy kwani alimkaribisha Dada yake kama vile alimkaribisha adui yake ndani ya nyumba. Suala hilo liliibua maswali mengi sana kwa Mr Aloyce pamoja na mgeni wao.
"Mama Eddy.. Nakuomba chumbani Mara moja..." Alisema Baba Eddy kisha akaingia chumbani. Mama Eddy alimfuata mumewe ili amsikilize kile anachotaka kumweleza.
"Mke wangu... Mbona unaniabisha kwa shemeji yangu?"
"Kivipi?"
"Dada yako amekuja lakini unamsalimia kama hutaki vile.. kwanini?" Aliuliza baba Eddy kwa mshangao.
"Nimejisikia tu.."
"Hapana mke wangu usiwe hivyo... Nakuomba basi onesha kumjali mgeni tena nduguyo wa damu.."
"Siwezi kumjali mchawi mkubwa yule..." Alisema mama Eddy akiwa anajishumburua midomo yake kwa dharau.
"Unasemaje? Dada yako mchawi kivipi?"
"Amemroga mwanangu..."
"Umejuaje au nawewe mchawi? Maana haiwezekani umtuhumu mwenzio mchawi wakati huna uhakika?" Alisema Baba Eddy kwa hamaki. Hakutaka kuamini kile alichokisa mkewe.
"Leo hii unaniambia mimi mchawi? OK sawa... " alisema Mama Eddy na kwenda sebuleni kwa hasira.
Alisimama wima akiwa ameshika mkono kiunoni huku akimtazama dada yake kwa dharau.
Dada yake alipigwa na butwaa sana, alibaki anamshangaa mdogo wake kwa vitendo vya dharau anavyomfanyia.
"Wewe!" Alisema Mama Eddy.
"Naomba utoke kwenye nyumba yangu.. Ulichomfanyia Eddy kinatosha..."
"Mimi?"
"Kumbe naongea na nani kama sio wewe mpumbavu..." Alisema Mama Eddy akidhihirisha chuki kubwa aliyonayo moyoni mwake. Eddy alimtazama mama yake kwa mshangao sana akiwa haelewi sababu ya mama yake kumfanyia unyama ule dada yake wa damu. Hakuna aliyefahamu ukweli kuwa yule hakuwa mama Eddy halisi.
"Mama... Mama mkubwa amekosa nini?"
"Hebu kelele huko na wewe.. Hujui kama huyu ndo aliyekuroga?"
"Sio huyu mama..." Eddy alimtetea.
"Hebu ondoka hapa.. Kwanza hayakuhusu.." Alifoka Mama Eddy.
"Sasa na mimi naondoka na mamkubwa.. Sibaki hapa?" Alisema Eddy.
Wakati huo Mr Aloyce alifika sebuleni pale na kuanza kumuomba msamaha mgeni yule asiye na hatia....
ITAENDELEA.....
Usikose
Read More...