RIWAYA YA MWANAFUNZI MCHAWI SEHEMU YA 23

RIWAYA: A WIZARD STUDENT ( MWANAFUNZI MCHAWI)
MTUNZI ENEA FAIDY

SEHEMU YA 23

...MR ALOYCE alolishikilia karatasi lile akiwa ameinamisha kichwa chake chini, mawazo yalimjaa tele kichwani mwake. Aliwaza achague lipi kati ya
Yale aliyoamriwa.
Alijiona ana mtihani mzito sana ambao alishindwa kufaulu kwa haraka. Akawaza ni heri amrudishe mkewe ili waendelee kushughulikia tatizo la mtoto wao wakiwa pamoja. 
"Namtaka mke wangu" alisema Mr Alloyce kwa sauti ya chini kisha ghafla akasikia sauti ya kicheko kikali kisha akatazama huku na kule bila kumuona mchekaji. Aliogopa kupita kiasi. Alitetemeka kama mtu aliyeshikwa na baridi Kali.
"Umechagua vyema maana ungetaka mwanao apone.. Ungepoteza kila kitu... Mkeo yupo kule Kule alikopotelea, hajafa ila tulitaka kumfundisha adabu tu kwa kulazimisha mambo." Ilisikika sauti ile iliyoambatana na mwangwi mkali.
Mr Alloyce alizidu kuogopa, akaangaza macho huku na kule lakini hakuona mtu. Woga ulimzidia sana baada ya karatasi alilokuwa ameshika mkononi kutoweka bila kujua limeenda wapi. Alitafuta pale sakafuni lakini hakuliona, akazidi kupigwa na butwaa. Maneno aliyoambiwa kuhusu mkewe yalizidi kujirudia kichwani mwake. Alihisi kama alikuwa akidanganywa tu, mkewe alishafariki na hawezi kurudi.
"Mtu alishafariki, nitakaaje nae tena? Mh! Dunia ina maajabu...!" Aliwaza Mr Alloyce.
"Kweli nitamwona mke wangu? Sijui niende Leo? Mh sasa hivi ni usiku sana!" Mr Aloyce aliwaza na kuwazua ubongoni mwake. Aliamua kuwa na subira, asiwe na papara. Aliamua kuisubiri kesho yake asubuhi ili aende sehemu ambayo mkewe alipotelea ili akamchukue.

Usiku ule ulikuwa mrefu sana kwa Mr Aloyce kwani hakuwa na hata lepe la usingizi, kila dakika alikuwa akiyafikiria matukio yote yaliyomtokea kwenye familia yake akahisi ndoto tu au mchezo wa kuigiza lakini ilikuwa kweli kabisa na alishuhudia kwa macho yake.
"Eddy! Mama yako mzima, tutaenda kumfata kesho asubuhi!" Mr Aloyce aliongea.
"Baba kweli?" Eddy alishtuka kusikia vile kwani sauti iliyokuwa ikisikika ndani mle na kumpa maelekezo Mr Alloyce, Eddy hakuisikia kabisa.
"Kweli mwanangu!"
Eddy aliachia tabasamu mwanana usoni kwake. Kwani hakika taarifa zile zilimfurahisha sana.
"Kesho asubuhi na mapema nitamfuata kule aliko.."
"Yuko wapi?" Kabla Mr Aloyce hajajibu swali la mwanae alishtushwa na mlio wa simu yake . simu iliita kwa sauti kutokea kwenye moja ya sofa pale sebuleni.
Mr Aloyce aliinuka na kuifuata lakini alipotazama kwenye kioo alishtuka kidogo.

***

Gari ilitembea kwa mwendo mrefu sana mpaka ilipofika eneo la uyole jijini Mbeya. Ndipo Bi Carolina alipoamua kuchukua simu yake na kupitisha vidole vyake laini vilivyonakshiwa kwa kucha nzuri zilizopakwa ranging nyekundu. Akatafuta namba Fulani kisha akapiga.
"Mume wangu uko wapi? Tumefika hapa uyole sio muda mrefu tutaingia hapo Nanenane!" Alisema Bi Carolina .
"Kwani upo na nani?" Ilisikika sauti ya upande wa pili.
"Aah bwana .. Tupo na abiria wenzangu... Niambie uko wapi?"
"Utanikuta Hapahapa Nanenane stendi .. Nimefika kitambo nakusubiri mke wangu!" Alisema mume wa Bi Carolina kisha simu ikakatika.

Majira ya saa moja na nusu hivi, Bi Carolina na Doreen walikuwa tayari wamewasili katika kituo cha mabasi cha Nanenane jijini Mbeya. Bi Carolina alionesha kumjali sana Doreen kwa kumkaribisha Binti huyo jijini Mbeya .
"Hii ndio Mbeya Doreen... Baridi hapa ndo kwake... Karibu sana"
"Asante mama!" Aliitikia Doreen kwa sauti ya upole sana akiwa ameachia tabasamu usoni pake.
Ghafla simu ya Bi Carolina ikaita, alipotazama ilikuwa namba ya mume wake akapokea kisha akasikiliza maelekezo . Akaelewa gari ya mumewe ilipo wakaelekea pale na kuikuta gari aina ya Prado ikiwa imepaki pembezoni mwa Barbara karibu na mango la kuingilia uwanja wa maonesho ya Nanenane.
Tabasamu pana kutoka kwa mwanaume mfupi kiasi, mnene, mwenye rangi ya kunde likamkaribisha Bi Carolina. Lakini punde tabasamu hilo la mume wa Bi Carolina likayeyuka ghafla baada ya kuona mkewe ameambatana na mtu asiyemfahamu.
"Mke wangu vipi?" Aliuliza mumewe huku akimtazama Doreen.
"Kwani vipi mume wangu?"
"Huyu nani?" Aliuliza
"Mgeni wetu.."
"Ndugu yako?"
"Hapana.. Tuachane na hayo.. Tutaongea tukifika" alisema Bi Carolina.
"Shkamoo..!" Alisalimia Doreen kwa upole sana . lakini mume wa Bi Carolina hakuitikia salamu ile.
"Mke wangu.. Usiniletee uchuro.. Huyu wa wapi..!" Alifoka
"Baba Pamela mume wangu.. Mbona uko hivo? Kuna ubaya gani kuja na mgeni?"

"Hakuna tatizo kama ungenijulisha.. Kwani ni ndugu yako?"
"Sio.. Ni mtoto tu nimeamua kumsaidia ana matatizo makubwa sana!" Alijitetea Bi Carolina lakini bado mumewe hakutaka kukubaliana nae. Hakumtaka kabisa Doreen.
"Tupeleke nyumbani..." Aliomba Bi Carolina.
"Ntakubeba peke yako.. Bila huyo mgeni wako.."
"Kuwa na roho ya utu mume wangu.. Tutamwachaje huyu mtoto barabarani hapa? Si ukatili huo.
"Nimesema simtaki mgeni wako nyumbani kwangu... Jifanye una huruma utaokota mpaka majini!" Alisema mume wa Bi Carolina kisha akafunga mlango wa gari na kuondoka zake huku akimwacha mkewe na Doreen palepale.
Bi Carolina alibaki akishangaa kitendo cha mumewe siku ile. Alimtazama Doreen aligundua kuwa analia, tena Amalia kwa uchungu sana.
"Usilie mwanangu tutaenda hata na daladala.." Alisema Bi Carolina kwa upole.
"Hapana mama.. Mi niache tu wewe nenda... Nisijekuharibu familia yenu bure" alisema Doreen huku akilia.
"Siwrzi kukuacha hapa Doreen, usiku sasa!" Alisema Bi Carolina.
"Hapana mama nenda!" Alisisitiza Doreen lakini Bi Carolina alizidi kumbembeleza waondoke wote. Ghafla simu ya Bi Carolina ikaita, akapokea.
"Mama Pamela! Ukitaka kuja na huyo mgeni wako, usifike kwangu... Ishia hukohuko..!"

ITAENDELEA

4 Comments